MASHABIKI wa Yanga Sc wanapaswa kuvuta subira. Mshambuliaji wao tegemeo, Clement Mzize, hatakuwepo uwanjani kwa muda mrefu baada ya kufanyiwa upasuaji wa goti uliokuwa ukimsumbua kwa muda mrefu. Habari kutoka ndani ya klabu hiyo zinasema kuwa nyota huyo atakuwa nje ya dimba kwa wiki nane hadi kumi, sawa na takribani miezi miwili kamili, jambo linalowatia hofu mashabiki wa Wananchi.
Mzize alipata jeraha hilo wakati akiitumikia timu ya Taifa ya Tanzania katika michuano ya mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ndani iliyofanyika hapa nchini. Awali, jeraha hilo lilionekana dogo na lilimweka nje kwa wiki tatu pekee, lakini hali ilizidi kuwa mbaya baada ya kurejea mazoezini na kutonesha sehemu hiyo.
Akizungumza na Waandishi wa habari, Ofisa Habari wa Yanga, Ali Kamwe, amethibitisha taarifa hizo na kueleza kuwa uongozi wa klabu umechukua hatua zote muhimu kuhakikisha nyota huyo anarejea akiwa imara zaidi.
“Ni kweli Mzize amefanyiwa upasuaji wa goti. Kwa mujibu wa daktari, atakuwa nje kwa wiki nane hadi kumi. Hivyo kwa kipindi hicho hatutakuwa na huduma yake uwanjani,” alisema Kamwe.
Kamwe aliongeza kuwa upasuaji huo ulifanyika baada ya vipimo vya kina kuonyesha kuwa tatizo lililomkumba Mzize lingeweza kuwa kubwa zaidi kama lingepuuzwa.
“Haikuwa rahisi kumshawishi mchezaji kukubali kufanyiwa upasuaji, lakini tumempa ushauri wa kitaalamu, tumemjengea hali ya kisaikolojia, na kwa msaada wa madaktari bingwa, hatimaye alikubali. Ni mchezaji mwenye roho ya ushindani, lakini afya ni muhimu zaidi,” alisisitiza.
Atakosa Mechi Nzito
Kwa mujibu wa ratiba, Mzize atazikosa mechi kadhaa muhimu ikiwemo michezo miwili ya Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya makundi dhidi ya timu za Far Rabat na Js Kyablie, pamoja na Dabi ya Kariakoo dhidi ya mahasimu wao wa jadi, Simba SC.
Hii ni pigo kubwa kwa kocha Pedro Concalves, ambaye alimtegemea Mzize kama chachu ya mabao msimu huu. Mzize ndiye alikuwa mchezaji kinara wa mabao kwa wazawa msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara, akifunga mabao 14, akimaliza nyuma ya Jean Charles Ahoua wa Simba aliyepachika 16.
Kutokana na kutokuwepo kwake, Pedro atalazimika kufanya mabadiliko katika safu ya ushambuliaji, huenda akimpa nafasi zaidi Prince Dube na Andy Boyeli, au kumrejesha kwenye mfumo mpya Celestine Ecua kama “false nine”.
🎯 Usipitwe!
Kuwa wa kwanza kupata habari za moto za michezo nchini Tanzania na duniani kwa ujumla, moja kwa moja kwenye barua pepe yako kutoka SportsLeo Bongo!
- ✅ Matokeo ya mechi
- ✅ Uchambuzi wa kina
- ✅ Habari za ndanii ya timu zako pendwa
✉️ Quality content, no spam. Unsubscribe anytime.
Mashabiki Watoa Neno
Kupitia mitandao ya kijamii, mashabiki wa Yanga wameonyesha hisia tofauti. Wengi wamemtakia Mzize nafuu ya haraka, huku wengine wakisisitiza klabu kuongeza nguvu kwenye dirisha dogo la usajili ili kujaza pengo lake.
“Mzize ni kipenzi cha Wananchi. Tumemwona akitoa uhai wake kwa jezi ya kijani na njano. Tunamtakia uponyaji wa haraka arudi akiwa imara zaidi,” aliandika shabiki mmoja kwenye ukurasa wa Yanga.
Madaktari Watuliza Hofu
Taarifa kutoka kitengo cha tiba cha klabu zinaeleza kuwa upasuaji huo umefanyika kwa mafanikio makubwa na mchezaji yuko katika hali nzuri. muda si mrefu ataanza programu za mazoezi mepesi ya kurejesha nguvu, chini ya usimamizi wa wataalamu wa tiba ya viungo.
“Upasuaji umeenda vizuri. Sasa tunasubiri kipindi cha awali cha wiki nne kabla ya kuanza mazoezi maalum ya kurejesha ufanisi wa goti,” alisema mmoja wa madaktari wa timu.
Kwa upande wake, Mzize ameahidi kurejea kwa nguvu zaidi.
“Ni kipindi kigumu lakini naamini nitarejea nikiwa bora zaidi. Asanteni kwa maombi na upendo wenu,” aliandika kwenye ukurasa wake wa Instagram.
Kwa mashabiki wa Yanga, ni wazi watamkosa sana kijana huyo mwenye kasi, nguvu na uwezo mkubwa wa kumalizia nafasi. Lakini kama alivyo msemo maarufu wa klabu hiyo, “Daima Mbele, Nyuma Mwiko,” Wananchi wanaamini kikosi chao kitavuka changamoto hii na kuendelea kutamba ndani na nje ya Tanzania.



