Site icon Sports Leo

Namungo Waifuata Raja Casablanca

Msafara wa watu 32 wa timu ya Namungo umeondoka Jijini Dar es Salaam usiku wa kuamkia leo Machi 8, kuelekea nchini Morocco katika mchezo wao wa kwanza wa makundi.

Namungo wawakilishi pekee katika michuano ya Kombe la Shirikisho, inatarajia kushuka dimbani Machi 10 kuwakabili Raja Casablanca katika mchezo wa kwanza wa kundi D.

Katika msafara huo Namungo imeondoka na wachezaji 22 benchi la ufundi sita pamoja na viongozi wanne tayari kwa mtanange huo unaotazamiwa kuwa na ushindani zaidi.

Mwenyekiti wa Namungo Hassan Zidadu ameaimba SA kuwa, msafara huo bado haujafika kwa sasa, lakini haujakumbana na kikwazo kama ilivyokuwa katika mchezo uliopita walipokwenda Angola kuwavaa Agosto.

“Wachezaji wetu wako poa na nimewasiliana nao muda si mrefu wako njiani, nitawatafuta baadae kujua kama wamefika, ila safari ni nzuri wameondoka na ndege ya abiria,”amesema.

Exit mobile version