Kaimu Kocha Mkuu wa Yanga Juma Mwambusi amesema dhamira ya kutwaa ubingwa wa ligi kuu msimu huu haijabadilika licha ya changamoto kadhaa zinazojitokeza.
Yanga imekaa kileleni mwa msimamo wa ligi kwa takribani miezi sita lakini bado wapo watu wanaamini Wananchi hawatakuwa na ubavu wa kutwaa ubingwa mbele ya watani zao Simba ambao wako nyuma kwa tofauti ya alama nne na michezo mitatu ya viporo
Akizungumza katika Mkutano na Wanahabari Makao Makuu ya klabu ya Yanga mapema leo, Mwambusi amesema dhamira ya kutwaa ubingwa iko palepale
“Dhamira yetu ya kutwaa ubingwa iko palepale. Nadhani hakuna mtu ambaye anaweza kusema Yanga haiko katika mpango wa kuwania ubingwa kwani mpaka sasa iko kileleni mwa msimamo wa ligi na timu nyingine zinafuatia,” alisema Mwambusi
Aidha kuhusu maandalizi ya kikosi chake kuelekea mchezo dhidi ya KMC utakaopigwa kesho Jumamosi katika uwanja wa Benjamin Mkapa, Mwambusi amesema wamejiandaa vya kutosha, amefanyia kazi baadhi ya changamoto zilizokuwepo awali na mashabiki watarajie kuona mabadiliko kuanzia mchezo huo
“Mpira ni sayansi kubwa sana, unaweza ukawa unalaumu mchezaji pasipo kujua sababu ni nini, makosa mengi yaliyokuwa yanafanyika mimi kama mwalimu ndiyo kazi yangu kuyarekebisha, tutarajie kuwa yanaweza kupungua kwa kiasi kikubwa”
Cc:Vanforsports