Klabu ya Azam Fc imelazimishwa sare ya bila kufungana na Prisons katika mchezo wa ligi kuu nchini uliofanyika katika uwanja wa Chamazi jijini Dar es salaam.
Licha ya patashika za hapa na pale lakini mpaka dakika ya 90 za mchezo zilimalizika kwa suluhu na kuifanya Azam fc kufikisha alama 38 katika michezo 21 huku Prisons ikifikisha alama 26 katika michezo 20 ikiwa katika nafasi ya nane ya msimamo wa ligi kuu nchini.
“Ulikuwa ni mchezo wa kutumia nguvu kubwa mwanzo mwisho jambo ambalo liliwafanya wachezaji wawe kwenye kasi hiyo muda wote.
“Licha ya kutengeneza nafasi ilikuwa ngumu kuzitumia kwa kuwa muda ambao unafika eneo la tukio tayari wapinzani wamefika, kipindi cha kwanza tulianza vizuri ila kipindi cha pili tukaamua kuongeza washambuliaji ili kubadili mbinu ila haikuwa bahati yetu.
“Bado tuna muda wa kufanya maboresho kwenye mechi zetu zijazo na tunaamini kwamba tutafanya vizuri kwa ajili ya mechi zetu zijazo,” Alisema Vivier Bahati kocha msaidizi wa Azam Fc.