Mshambuliaji Ditram Nchimbi amekosekana katika mazoezi ya timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ yanayofanyika leo asubuhi katika Uwanja wa Benjamini Mkapa.
Awali katika mazoezi ya jana Jumanne Machi 9, mchezaji huyo hakufanya kabisa mazoezi na alikuwa amekaa pembeni akiangalia wenzake.
Kocha Kim Poulsen pamoja na daktari wa timu , Richard Yomba walikuwa wakizungumza na kumuita mchezaji huyo na kuonyesha kuumia misuli ya paja.
Katika mazoezi ya leo Jumatano asubuhi mchezaji huyo hajaonekana kabisa hata kuangalia mazoezi kama ilivyokuwa jana jioni.
Mtu wa karibu na mchezaji huyo amesema kwamba, Nchimbi baada ya kuonekana hali yake inahitaji kupumzika wamemuondoa kikosini.
“Jana mbona baada ya kutoka mazoezini alienda kambini kwao akachukua vifaa akarudi nyumbani, hayupo tena na timu.”
Stars inajiandaa kucheza mechi mbili za kirafiki dhidi ya Kenya Machi 15 na Machi 18 kisha baada ya hapo wataenda kucheza mechi ya kufuzu Afcon dhidi ya Equatorial Guinea, Machi 25.