Ndanda FC imekabiliwa na ukata wa kifedha tangu serikali iliposimamisha ligi zote Tanzania Bara kutokana na janga la Corona hivyo klabu hiyo imeliomba Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) liwakopeshe fedha zitakazowasaidia katika uendeshaji pia kumalizia michezo iliyobaki ya Ligi Kuu Bara.
Ndanda klabu ambayo imekuwa ikiendeshwa kwa michango ya wanachama,wadau na mara kwa mara wamekuwa wana hali mbaya kiuchumi huku mara kadhaa wakikiri kushindwa kulipa mishahara ya wachezaji wao.
Selemani Kachele ambaye ni katibu mkuu wa klabu hiyo amesema amesikia kuwa ligi kuu bara inaweza kurejea hivi karibuni kama hali ya mambo ikiwa vizuri, japo ni jambo la kushukuru lakini kwa upande wao uchumi sio mzuri.
“Kama mnavyojua kuwa klabu hii inaendeshwa kwa michango ya wanachama, hivyo tunaiomba TFF na Bodi ya Ligi kama itafikia uamuzi wa kuirejesha ligi basi watusaidie kutukopesha fedha zitakazotusaidia kuiendesha klabu yetu kumalizia michezo iliyobaki.”alisema Kachele
Katika msimamo wa Ligi Kuu Bara, Ndanda fc inashika nafasi ya 16 baada ya kujikusanyia pointi 31 katika michezo yake 29.