Kampuni ya Vodacom imetangaza kujitoa kuendelea kudhamini ligi kuu ya Tanzania Bara baada ya kupata hasara kubwa katika kipindi cha mwaka mmoja kutokana na ripoti yao ya fedha.
Kwa mujibu wa ripoti ya fedha ya mwaka 2020/21, Vodacom imetangaza kupata hasara ya Tsh Bilioni 30 huku asilimia kubwa ya hasara hiyo ikichagizwa na matumizi makubwa ya kampuni hiyo ikiwemo udhamini wa ligi kuu nchini.
Ofisa Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo, Hisham Hendi amesema imekuwa ni fahari kubwa kwao kudhamini ligi kuu ya Tanzania kwa kipindi cha miaka 10 Lakini kutokana na mwenendo wa ufanisi wa kampuni hawataendelea na udhamini huo.
“Tunafurahia ubia na tunapenda, ligi imekuwa ikiitwa jina letu Lakini kwa kampuni ambayo imetengeneza hasara, leo usipoweza kuinuka juu lazima uangalie gharama zako”Alisema Hendi huku akimalizia kwamba “Katika mazingira hayo magumu lazima uchukue uamuzi mgumu,” Hisham alinukuliwa na gazeti la Mwananchi