Baada ya kocha msaidizi wa klabu ya Yanga sc Juma Mwambusi kuomba kujiweka kando kutokana na matatizo ya kiafya majina matano yanatajwa kuwa mikononi mwa mabosi wa timu hiyo kurithi mikoba ya kocha huyo.
Kwa sasa Yanga ipo chini ya Kocha Mkuu, Cedric Kaze huku akiwa bila msaidizi na jukumu la kuchagua msaidizi lipo mikononi mwake ambapo mpaka sasa hajasema jina la msaidizi huyo.
Mwambusi aliomba kujiweka kando wakati wa mashindano ya Kombe la Mapinduzi lililofanyika visiwani Zanzibar na Yanga ilisepa na taji hilo kwa mara ya pili baada ya kuifunga Simba sc kwa penalti 4-3 baada ya dakika 90 kukamilika kwa sare ya bila kufungana.
Iliwekwa wazi rasmi Januari 21 na Mwenyekiti wa Klabu ya Yanga, Mshindo Msolla kuhusu suala hilo la Mwambusi ambaye alikuwa na maelewano makubwa na Kaze.
Miongoni mwa wanaotajwa kuingia anga za Yanga ni pamoja na Mecky Maxime, Kocha Mkuu wa Klabu ya Kagera Sugar, Maalim Saleh ‘Romario’,.
Nizar Khalfan ambaye kwa sasa anaifundisha Klabu ya African Lyon ambayo inashiriki Ligi Daraja la Kwanza.
Adolf Richard ambaye alikuwa Kocha Mkuu wa Klabu ya Tanzania Prisons na aliweza kuiongoza kwa mafanikio msimu uliopita kwa kuwa ilimaliza ndani ya 10 bora.
Ramadhani Nswanzurimo ambaye aliwahi kuwa Kocha Mkuu wa Mbeya City pia aliifundisha Klabu ya Singida United kwa sasa yupo huru ila yupo ardhi ya Bongo.