Klabu ya Arsenal imekubali kipigo cha mabao 2-0 dhidi ya Liverpool katika mchezo wa kombe la Carabao uliofanyika katika uwanja wa Emirates jijini London ukiwa ni mchezo wa marudiano baada ya kutoka suluhu katika mchezo wa awali katika uwanja wa Anfield.
Mabao mawili ya Diogo Jota dakika za 19 na 77 yalitosha kuipeleka Liverpool fainali baada ya kumalizia kazi nzuri za beki Trent-Alexander Anord aliyetoa pasi nzuri za mabao kwa staa huyo.
Mikel Arteta ameingia vinywani mwa wadau wa soka baada ya kumchezesha Thomas Partey ambaye saa chache alikua ametoka kucheza michuano ya Afcon akiwa na taifa lake la Ghana na kusababisha kupata kadi nyekundu dakika 16 tangu aingie uwanjani.
Pamoja na kuwakosa mastaa Sadio Mane na Mo Salah walioko katika michuano ya mataifa ya Afrika Liverpool ilicheza vizuri kiasi cha kupata ushindi huo huku ikitarajia kuvaana na Chelsea katika mchezo wa fainali utakaofanyika katika uwanja wa Wembley jijini London Februari 27.