Mashabiki wa Simba Sc walikuwa na kazi moja tu Juzi ya kujitokeza uwanja wa taifa Dar na kuwajibu watani wao Yanga kuwa ‘Nyie mna Mghana sisi tuna Mbrazili mfunga mabao’
Waliipata jeuri hiyo baada ya kiungo wao Gerson Fraga raia wa Brazil kufunga mabao mawili na kuwapa pointi tatu Simba mbele ya Coastal Union.
Fraga alifunga bao la kwanza kwa kichwa akiunganisha krosi ya Clatous Chama dakika ya saba kipindi cha kwanza huku bao la pili alimalizia kirahisi na mpira uliopigwa na Hassan Dilunga dakika ya 78 na kuifanya Simba kuibuka kifua mbele.
Simba wanazidi kukaa kileleni wakiwa na pointi 47 baada ya kucheza mechi 18 na kushinda mechi 15 huku wakiiacha Yanga pointi 19 ikiwa imecheza mechi 15.