Ni nguvu ya kikosi cha michuano ya kimataifa ndio imetumika kuwamaliza Geita Gold Fc katika mchezo wa ligi kuu baina ya Yanga sc na timu hiyo ambao umemalizika kwa Yanga sc kuibuka na alama tatu katika mchezo huo mkali na wa kusisimua uliofanyika katika uwanja wa Azam Complex Chamazi jijini Dar es salaam.
Yanga sc ikianza bila straika Fiston Mayele ilikubali kufungwa bao la mapema na Elias Maguli dakika ya 20 baada ya kumzidi maarifa beki Dickson Job lakini kipindi cha pili Yangas sc walirudi na akili ya kikubwa na kufanikiwa kumaliza mchezo na ushindi wa 3-1 huku wakishambulia mwanzo mwisho.
Dakika za 49 na 50 ziliwapatia Yanga sc mabao mawili kupitia kwa Kennedy Musonda aliyemalizia kwa kichwa krosi ya Joyce Lomalisa huku Mzize akifunga kwa kumalizia shuti la Musonda lililopanguliwa na kipa wa Geita Gold Fc na pia akili ya ziada ya winga Jesus Moloko iliwapatia Yanga sc bao la tatu dakika ya 70 na kuumaliza mchezo huo.
Yanga sc sasa imefikisha alama 65 ikicheza michezo 24 ya ligi kuu nchini huku ikiwasubiri Kagera Sugar kisha Simba sc katika michezo ya ligi kuu nchini.