Uongozi wa Klabu ya Yanga sc umethibitisha kupokea majibu kutoka Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Michezo (CAS) kuhusu kesi yao namba CAS 2025/A/11298 iliyoifungua kupinga maamuzi ya bodi ya ligi nchini kughairisha mchezo namba 184 uliokua ufanyike machi 20 2025 dhidi ya Simba Sc.
Baada ya shauri hilo ambalo Cas wamelitolea majibu ambapo Yanga Sc imeelekezwa kurudi kwenye Kamati za ndani za soka hapa nchini kabla ya kuwasilisha shauri lao kwa hatua za rufaa kimataifa.
Hata hivyo uongozi wa Klabu hiyo umeeleza kuwa hauna imani kabisa na Mamlaka za soka nchini kutokana na kile walichokiita uonevu, uvunjaji wa kanuni na upendeleo wa wazi unaoendelea kufanywa dhidi ya baadhi ya Timu na Kwa sababu hiyo Yanga imesisitiza haitapeleka shauri hilo kwenye Mamlaka hizo za ndani wanazodai kuwa siyo za haki.
Katika msimamo wao klabu hiyo pia imeweka wazi kuwa haipo tayari kushiriki mchezo wa Ligi Kuu namba 184 kwa namna yoyote ile na imetoa wito kwa Wanachama na Mashabiki wake kuwa tayari kupigania haki yao ili kukomesha dhulma na kusaidia katika kujenga misingi ya haki na usawa kwa maendeleo ya soka la Tanzania.