Home Soka Singida Black Stars Kuwakabili Mashujaa FC Kesho Jijini Dar

Singida Black Stars Kuwakabili Mashujaa FC Kesho Jijini Dar

Gamondi na Masalanga Watoa Tahadhari

by Dennis Msotwa
0 comments

Klabu ya Singida Black Stars kesho Jumanne itashuka dimbani kuivaa timu ya Mashujaa FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC utakaopigwa kwenye Uwanja wa KMC Complex, Kinondoni jijini Dar es Salaam. Mchezo huu unatarajiwa kuwa wa ushindani mkubwa hasa ukizingatia matokeo ya awali ya timu zote mbili pamoja na maandalizi yao kuelekea msimu huu wa 2025/26.

Mashujaa FC, ambao ni miongoni mwa timu mpya zinazopanda chati kwa kasi, wameshacheza michezo miwili msimu huu wakiwa nyumbani na hadi sasa wameruhusu bao moja pekee – jambo linalowafanya kuonekana kama timu imara hasa katika safu ya ulinzi. Licha ya kuwa wapya kwenye Ligi Kuu, Mashujaa wameongeza nguvu kwenye kikosi chao kwa kuwasajili washambuliaji hatari, ambao tayari wameanza kuonyesha uwezo wao uwanjani.

Akizungumza na waandishi wa habari kuelekea mchezo huo, Kocha Mkuu wa Singida Black Stars, Miguel Ángel Gamondi, amesema wanaiheshimu Mashujaa kama timu mpya yenye ubora, lakini wamejipanga ipasavyo kuhakikisha wanapata matokeo mazuri jijini Dar.

banner

“Tunajua Mashujaa wameanza msimu kwa nidhamu ya kiuchezaji, wameongeza washambuliaji wazuri na wamekuwa na ulinzi madhubuti. Ingawa mechi zao zote mbili zimechezwa nyumbani, wameonesha kuwa si timu ya kubeza. Mtindo wao wa uchezaji hautofautiani sana na timu nyingine ambazo tumekutana nazo, hivyo tumejipanga vizuri kuwaziba mianya na kuhakikisha tunapata pointi tatu,” alisema Gamondi kwa kujiamini.

Singida Black Stars walimaliza msimu uliopita katika nafasi nzuri na kwa sasa wamekuwa wakipambana kurejesha nafasi yao kama moja ya timu tishio nchini. Wanajivunia kikosi kilichoboreshwa, benchi la ufundi imara, na morali nzuri kutoka kwa mashabiki wao waliopo ndani na nje ya mkoa wa Singida.

Kwa upande wa wachezaji, golikipa Hussein Masalanga, ambaye amekuwa na kiwango bora tangu msimu uanze, amesema wachezaji wa Singida Black Stars wako tayari kwa pambano hilo na wanajua wanachokikabili, ingawa hawataichukulia Mashujaa FC poa.

“Tumefanya maandalizi ya kutosha kwa mchezo huu. Tunawaheshimu Mashujaa kwa sababu ni timu nzuri na wameonesha hilo kwenye mechi zao zilizopita. Lakini sisi kama wachezaji wa Singida tupo tayari kupambana kwa ajili ya ushindi. Tunajua changamoto za kucheza ugenini lakini tuna imani na uwezo wetu,” alisema Masalanga.

Mchezo huu unakuja wakati Ligi Kuu ikiwa katika hatua za mwanzo, ambapo kila timu inahitaji alama za kujiweka sawa kwenye msimamo. Kwa Singida Black Stars, ushindi utawasaidia kuongeza morali ya kikosi chao na kuwaweka kwenye nafasi nzuri ya kuendelea kupambana kwa nafasi za juu kwenye msimamo wa ligi.

Kwa Mashujaa, ambao bado hawajacheza mechi yoyote ugenini, hii itakuwa fursa ya kupima uwezo wao nje ya Kigoma na kuona namna wanavyoweza kujimudu dhidi ya timu zilizothibitisha ubora wake, kama Singida Black Stars.

Mashabiki wa soka jijini Dar es Salaam wanatarajiwa kujitokeza kwa wingi kushuhudia mchezo huu wa kuvutia, huku wakifuatilia namna kila timu itakavyotumia mbinu na mikakati yake kuhakikisha inapata alama muhimu.

You may also like

Leave a Comment

Sportsleo Bongo ni tovuti ya kwanza na bora zaidi ya michezo nchini Tanzania, ikileta habari kwa Kiswahili, matokeo ya moja kwa moja, tetesi, na taarifa muhimu kuhusu soka, ndondi, riadha na michezo mingine ndani na nje ya Tanzania.

Edtior's Picks

Latest Articles

Sportsleo Bongo Developed and designed by Mediapix Limited