Morocco Yaanza na Ushindi Afcon

RABAT, Morocco Katika mchezo wa ufunguzi wa Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025, wenyeji Morocco walijipatia ushindi wa 2–0 dhidi ya Comoros, mchezo uliochezwa usiku wa Jumapili kwenye uwanja wa Prince Moulay Abdellah mbele ya mashabiki wengi waliokusanyika.
Huu ulikuwa ni mchezo wenye shinikizo kubwa kwa Morocco, ambao walionekana kuanza polepole kabla ya hatimaye kupata muunganiko wa nguvu na ustadi wao wa juu kipindi cha pili. Matokeo hayo yamewaweka Morocco kileleni mwa kundi A huku wakitaka kusonga mbele hadi hatua ya 16 bora “round of 16”.
Diaz Akosa Penati
Mchezo ulianza kwa mwendo wa haraka na Morocco wakionyesha nia ya dhati ya kufunga mapema zaidi na hatimaye Dakika ya 10, Morocco walipata penati baada ya mshambuliaji Brahim Diaz kuangushwa ndani ya eneo la hatari. Hata hivyo,mshambuliaji huyo alikosa baada ya kipa wa Comoros, Yannick Pandor, kufanya kitendo cha kukataa shuti hilo kwa ustadi mkubwa.

Comoros, taifa dogo la visiwa vya Bahari ya Hindi, walicheza kwa nidhamu kubwa katika dakika za mwanzo, wakiweka mabeki wengi nyuma ya mpira na kujaribu kuzima mashambulizi ya wenyeji. Hii ilisababisha Morocco kushindwa kutengeneza nafasi nyingi za wazi kipindi cha kwanza. Hadi mapumziko, timu zote zilikamilisha dakika 45 bila kufungana bao lolote.
Changamoto Ya Majeraha Yaanza Mapema kwa Wachezaji
Mapema kipindi cha kwanza, Romain Saiss, nahodha wa Morocco, alibadilishwa kutokana na jeraha baada ya kuguswa kidogo na mchezaji wa Comoros, jambo lililowachanganya wachezaji na mashabiki. Hali hii ilionyesha changamoto kwa Morocco kuendelea na mchezo chini ya shinikizo kubwa la mashabiki na matarajio yao ya ushindi.
Kocha wa Morocco, Walid Regragui, alikiri mwendo wa mchezo ulikuwa mgumu na shinikizo la mchezo kutaka mabao lilizidi kuwa kubwa. Aliongeza kwamba ilibidi wafanye marekebisho kipindi cha mapumziko ili kuboresha muundo wa mchezo na kuongeza kasi ya mashambulizi.

Brahim Diaz Aonyesha Ustaa
Kipindi cha pili kilianza na Morocco wakionyesha ustadi wao wa kipekee. Dakika ya 55, baada ya shambulizi kali, beki Noussair Mazraoui aliweka pasi nzuri ndani ya kisanduku cha Comoros, na Brahim Diaz, staa wa Real Madrid, akafunga bao la kwanza kwa usahihi wa hali ya juu. Mashabiki walililia kwa furaha sehemu mbalimbali za uwanja huku Morocco wakipewa nguvu mpya ya kushangilia kwa mashabiki
Baada ya dakika kadhaa za shambulizi la mara kwa mara, dakika ya 74, Ayoub El Kaabi aliyekuwa ameingia kama mchezaji mbadala, alipiga shuti la ajabu la overhead bicycle kick lililopa wenyeji bao la pili. Shuti hili lilikuwa moja ya matukio makubwa ya usiku huo, na Morocco wakaanza kujiamini zaidi kwamba ushindi haukutawaliwa tena.
El Kaabi, staa mwenye uzoefu mkubwa, ameonyesha mara kwa mara uwezo wake wa kufunga mabao ya kuvutia sio tu kwa Morocco lakini pia katika michuano ya ligi na Kimataifa.
Kiwango cha Kipa wa Comoro Chashangaza
Hata baada ya kufungwa mabao, Comoros hawakuacha kupambana. Walijaribu kurudi mchezoni na hata waliweza kutengeneza nafasi chache za kushtua huku Kipa Yannick Pandor aliendelea kuonyesha uwezo mkubwa kwa kuzuia mipira mikali mara kadhaa.

Hatimaye ushindi ulienda kwa Morocco pamoja na jitihada za Comoro kutaka kusawazisha lakini bahati haikua upande wao licha ya kupambana sana.
Morocco sasa inapania kupanua rekodi yao ya ushindi na kuonyesha kuwa wanaweza kushindana kwa nguvu dhidi ya washindani wao Afrika na kimataifa. Wachezaji na benchi la ufundi wanatarajiwa kufanya kazi zaidi kuongeza muundo wa mchezo na kuhakikisha mafanikio katika mechi zijazo.
