Nyota wa Twiga Stars na Brighton & Hoves ya England, Aisha Masaka ametoa neno la shukrani baada ya kushinda tuzo ya mwanamichezo bora wa kike mwaka 2024, katika usiku wa tuzo za Baraza la michezo la Taifa uliofanyika Jumapili Juni Mosi 2025.
Masaka ambaye ni mara yake ya kwanza kushinda tuzo hiyo, ametoa ushauri kwa wanamichezo wa kike chipukizi, akiwataka wajitume huku akigusia mipango ya tamasha lake litakalofanyika Juni 8 chini ya ‘Aisha Masaka Foundation’
“Nashukuru sana kwa tuzo na ndio maana tumeandaa tamasha maalumu kuwashukuru wote waliotusaidia na tunawakaribisha wadau wa soka nchini kuja kutusapoti ili turudishe kwa jamii ambapo pesa itakayopatikana tutakwenda kujenga vyoo huko lindi hivyo nawakaribisha sana Kmc Complex kwa maana bei za tiketi ni nafuu”.Alisema mchezaji huyo wa zamani wa klabu ya Yanga Princess ya Dar es Salaam.
Aisha mzaliwa wa Singida alianza soka katika klabu ya Yanga Princess kisha akapata dili nchini Sweden katika klabu ya Bk Hacken FF ambapo baada ya miaka miwili alijunga na klabu ya Brighton & Hove albion anapocheza mpaka sasa.